Wednesday, October 22, 2014

MFUKO WA TAIFA WA BIMA YA AFYA NHIF WASHIRIKI WIKI YA VIJANA KITAIFA TABORA

Meneja mwandamizi wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya kanda Bw.Emmanuel Adina akijaribu kutoa maelezo kuhusu mfuko wa afya ya jamii CHF na tiba kwa kadi maarufu TIKA kwa mmoja kati ya wananchi waliotembelea Banda la maonesho la NHIF wakati wa wiki ya vijana kitaifa mkoani Tabora.
Mmoja kati ya maafisa wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya akimpima Uzito na Urefu mmoja kati ya wananchi wa Tabora waliotembelea Banda la NHIF na kupima afya zao wakati wa wiki ya vijana  kitaifa mkoani Tabora.
Afisa Masoko na Elimu kwa Umma  wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya  NHIF Bi.Catherine Kameka akitoa maelezo kwa mwandishi wetu wakati alipotembelea Banda la Mfuko huo.
Baadhi ya wananchi walijitokeza kupima afya zao


Baadhi ya maafisa wa NHIF wakiendelea kufuatilia taarifa mbalimbali kwenye mtandao ambazo wanazitumia katika maonesho hayo kuielimisha jamii umuhimu wa kutunza afya zao.
Banda la Chama cha msalaba mwekundu
Mabanda mbalimbali ya maonesho katika wiki ya vijana kitaifa mkoani Tabora





PROF.TIBAIJUKA AFANYA ZIARA YA KUSHITUKIZA USIKU CHUO CHA ARDHI TABORA

Waziri wa ardhi,Nyumba na Maendeleo ya Makazi  Prof.Anna Tibaijuka akikagua moja ya mabweni ya wanafunzi wa Chuo cha Ardhi Tabora ambapo ziara hiyo ameifanya kwa kushitukiza majira ya saa moja usiku.

Prof.Tibaijuka akimpongeza mkuu wa Chuo cha Ardhi Tabora Bw.Biseko Musiba kwa kukisimamia vizuri chuo hicho licha ya ukosefu wa masuala mbalimbali ya msingi ikiwa ni pamoja na upungufu wa watumishi,vifaa vya kufundishia kama kompyuta na vinginevyo.
Prof.Tibaijuka alitembelea pia maktaba ya chuo hicho ambacho haina kompyuta kama nyenzo muhimu za kujifunzia wanachuo.
Prof.Tibaijuka alipata fursa ya kuzungumza na wanafunzi na walimu na watumishi wa chuo hicho.
Mkuu wa Chuo cha Ardhi Tabora Bw.Biseko Musiba akisoma taarifa fupi ya chuo hicho na namna chuo kinavyokabiliana na changamoto mbalimbali katika kuhakikisha kinatoa wataalamu wenye fani inayojitosheleza kwenye masuala ya ardhi nchini.




WANAFUNZI WA SHULE ZA SEKONDARI TABORA WAUSHAURI MFUKO WA TAIFA WA BIMA YA AFYA KUHAMASISHA MASHULENI

RAIS KIKWETE ALIPOTEMBELEA BANDA LA BIMA YA AFYA WAKATI WA WIKI YA VIJANA TABORA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dr.Jakaya Kikwete akisisitiza jambo kwa maafisa wa NHIF wakati alipotembelea banda la maonesho la Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya  NHIF wakati wa wiki ya Vijana iliyofanyika kitaifa mkoani Tabora.
Rais Kikwete akisalimiana na baadhi ya maafisa wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya


Rais Kikwete alishuhudia baadhi ya wananchi wakipata huduma za upimaji wa magonjwa mbalimbali shughuli iliyokuwa inafanywa na Mfuko huo wa Bima ya Afya ambapo idadi kubwa ya watu ilijitokeza kupata huduma hiyo.
Baadhi ya maafisa wa Mfuko wa Bima ya Afya wakiwa na Meneja mwandamizi wa Mfuko wa Bima ya Afya kanda ya Magharibi Bw.Emmanuel Adina






SERIKALI YAFUTA MAFUNZO YA UALIMU NGAZI YA CHETI


Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Dr.Shukuru Kawambwa akizungumza wakati alipotembelea Shule ya Sekondari ya Tabora Wavulana

 

SERIKALI imefuta kozi zote za mafunzo ya ualimu ngazi ya cheti kuanzia mwaka huu kwa lengo la kuboresha kiwango cha elimu hapa nchini.

Tamko hilo limetolewa jana na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Dr Shukuru Kawambwa alipokuwa akizungumza na wanachuo wa Chuo Cha Ualimu Tabora kilichoko katika Manispaa ya Tabora.

Alisema kuanzia mwaka huu serikali imeamua kuondoa mafunzo ya ualimu ngazi ya cheti ikiwa ni mkakati maalumu wa kuanza kuboresha kiwango cha elimu hapa nchini ambapo waalimu watakaoajiriwa kufundisha shule za msingi na sekondari watatakiwa kuwa na elimu ya kiwango cha diploma na kuendelea.

Alieleza kuwa kuanzia sasa wizara yake inataka ubora wa elimu upatikane kutokana na ubora wa waalimu huku akibainisha kuwa waalimu wote watakaoajiriwa katika shule za msingi na sekondari kuanzia mwaka huu lazima wawe na elimu ya kiwango cha kuanzia diploma na kuendelea huku akifafanua kuwa wale wasiokuwa na diploma watapewa fursa ya kujiendeleza bila tatizo lolote.

Aidha alisema waalimu wa shule za msingi na sekondari na wahitimu wa kidato cha sita waliopata daraja la 1-3 waliochaguliwa kujiunga na kozi maalumu ya mafunzo ya ualimu tarajali ngazi ya cheti wote watapelekwa vyuoni kupata masomo ya ngazi ya diploma katika vyuo maalumu vilivyoandaliwa.

Aidha katika kuhakikisha mpango huu mpya unatekelezwa, Dr Kawambwa alisema wizara inaandaa waraka maalumu wa maelekezo utakaotumwa kwa wakurugenzi wote wa halmashauri zote hapa nchini.


Akijibu swali la wanafunzi wa chuo hicho waliotaka kujua ni kwa nini mda wa  kwenda kufanya mazoezi (BTP) umepunguzwa na kuwa wiki 3 badala ya siku 60, waziri alisema utaratibu huo ni wa dharura tu kutokana na uhaba wa fedha ila akaahidi kuwa watajitahidi kurekebisha hali hiyo kadri hali ya kifedha itakavyoruhusu.

Aidha kuhusiana na ombi la kuongezwa posho ya mazoezi kutoka sh 4500 wanazolipwa sasa wanafunzi hao wa mafunzo ya ualimu hadi sh 7500 wanazolipwa wanafunzi wa ngazi ya shahada, waziri aliahidi kulifanyia kazi kutokana na bajeti ya wizara yake itakavyokuwa.

Aidha waziri aliwataka wanafunzi wote wa vyuo vya ualimu kuhakikisha wanafaulu masomo yao yote wanayofundishwa chuoni ili waweze kuajiriwa na serikali vinginevyo watalazimika kukaa benchi.

‘Wakati naingia wizarani  nilisema sitaajiri waalimu waliofeli na nitaendelea na msimamo huo huo kwa nia njema kabisa, jitahidini kufaulu masomo yenu yote ya kufundishia na yale ya ziada vinginevyo hatuwapi kazi, alisema Dr Kawambwa.

Tuesday, October 21, 2014

455 WAHITIMU CHUO KIKUU AMUCTA -TABORA

 

www.kapipijhabari.com



WANAFUNZI 455 wamehitimu mafunzo ya kozi mbalimbali ikiwemo shahada ya
uzamili katika Chuo Kikuu cha Askofu Mkuu Mihayo Tabora (AMUCTA)
ambacho ni Chuo Kikuu kishiriki cha Mtakatifu Augustino katika
mahafali ya pili ya Chuo hicho yaliyofanyika jana mjini Tabora.

Akizungumza katika mahafali hayo Mwenyekiti wa bodi ya Chuo hicho
Mhashamu Baba Askofu Mkuu Paulo Ruzoka ambaye pia ni Askofu wa Jimbo
Kuu la Tabora aliwataka wahitimu hao kuwa kioo katika jamii na
kutekeleza majukumu yao kwa weledi mkubwa ili kukiwakilisha vyema chuo
hicho.

Askofu Ruzoka aliwakumbusha kuwa elimu waliyopata ni kwa faida ya
Watanzania wote hivyo wanapaswa kuitumia kwa manufaa yao na jamii
inayowazunguka mahali popote watakapokuwa sambamba na kushiriki kazi
zote kwani jamii ina mategemeo makubwa sana kwao.

Kuhusu mchakato wa katiba mpya, Askofu Ruzoka aliwakumbusha wahitimu
hao kusoma kwa makini katiba iliyopendekezwa ili zoezi la kupiga kura
litakapofika wafanye uamuzi sahihi na sio ushabiki tu wa makundi.

Aidha aliwakumbusha kuwa ili wawe na sifa ya kupiga kura ni lazima
wajiandikishe kwenye daftari la kudumu la wapiga kura wakati
utakapofika.

Askofu Ruzoka alisisitiza zaidi wahitimu hao kuhamasishana wao kwa wao
wakiwemo wananchi wenye umri wa kupiga kura kwa pamoja wajiandikishe
kupiga kura ili haki yao ya msingi isipotee bure.

Aliwataka kuwa waelimishaji wazuri kwa jamii katika masuala mbalimbali
yanayolenga mustakabali wa maendeleo ya taifa kwa ujumla sambamba
kujiendeleza zaidi kielimu.

Katika hotuba yake Mkuu wa Chuo Kikuu cha Askofu Mkuu Mihayo Tabora
(AMUCTA) Padre Dr. Juvenalis Asantemungu alipongeza jitihada za bodi
na uongozi mzima wa chuo hicho ambazo zimekiwezesha kukua kwa kasi na
ongezeko kubwa la wanafunzi, wahadhiri na kozi mbalimbali.

Akizungumzia mkakati wa kuinua kiwango cha elimu hapa nchini Dr
Asantemungu alisema Chuo hicho kinampango wa kuanzisha kozi ya diploma
ya elimu kwa walimu wanaofundisha shule za msingi kozi ambayo itakuwa
inafundishwa siku za Ijumaa na Jumamosi ili kutoa fursa kwa walimu hao
kusoma huku wakiendelea na kazi zao lengo likiwa kuiwezesha serikali
kutimiza mpango wake wa ‘matokeo makubwa sasa’.

Akitoa takwimu za wanafunzi waliohitimu mwaka huu alisema wanafunzi 18
wamehitimu Shahada ya Uzamili katika Utawala wa Elimu na Mipango
(Maters of Education Management and Planning) na 345 Shahada ya kwanza
ya Elimu Jamii na Ualimu (Bachelar of Arts with Education).

Wahitimu wengine ni 48 wa Shahada ya kwanza ya Sosholojia (Bachelar of
Arts in Sociology) na 37 waliohitimu kozi za Astashahada katika fani
za Uongozi wa Biashara, Ununuzi na Ugavi, Ukutubi na Utunzaji wa
kumbukumbu.

Aidha Dr.Asantemungu aliwasisitiza kuwa mabalozi wazuri huko waendako
na wazidi kujiendeleza zaidi kwa shahada za Uzamili na Uzamivu kwa
kuwa elimu ni chachu kuu ya kuleta maendeleo ya kiuchumi na kijamii
ulimwenguni kote huku akisisitiza uvumilivu wanapopambana na
changamoto katika safari yao kimaisha.