Friday, January 17, 2014

NHIF’ KUJENGA JENGO LA KITEGA UCHUMI TABORA

Mwakilishi wa Mkurugenzi wa mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya NHIF ambaye pia ni kaimu Mkurugenzi wa CHF nchini  Bw.Athumani Rehani akiwasilisha salamu za NHIF katika mkutano huo wa wadau ambapo alieleza kuwa mfuko huo upo tayari kushirikiana  kwa karibu katika kuchangia Maendeleo ya mkoa wa Tabora huku ukiiomba Serikali ya mkoa huo kuwapatia eneo ambalo mfuko utawekeza kwa kujenga Jengo la Ghorofa Sita.

 
 Na Lucas Raphael,Tabora

MFUKO wa Taifa wa Bima ya Afya -NHIF, umedhamiria kujenga jengo la kitega uchumi mkoani Tabora litakalokuwa na ghorofa sita.

Hayo yalibainishwa na Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa NHIF Rehan Athuman katika semina ya wadau mbalimbali wa mfuko huo iliyofanyika juzi katika ukumbi wa Mtemi Isike Mwana Kiyungi mkoani humo.

Alisema NHIF imekusudia kuleta mageuzi makubwa katika utoaji wa huduma za afya kwa wanachama wake hapa nchini na katika siku za usoni mfuko huo una mpango wa kujenga jengo la kisasa katika mkoa wa Tabora litakalokuwa na ghorofa sita ili kurahisisha utoaji huduma.

Aidha alisema mfuko huo umedhamiria kuboresha na kupanua wigo wa utoaji huduma za afya katika mikoa yote hapa nchini ili wanachama wake waweze kujivunia ubora wa huduma hizo sambamba na kusajili wanachama wapya kwa wingi zaidi.

Ili kuboresha huduma za mfuko wa afya ya jamii mkoani Tabora na kusogeza huduma hizo karibu na wananchi  NHIF inakusudia pia kujenga jengo la kituo cha matibabu katika Manispaa hiyo kwa lengo la kupanua wigo wa huduma hizo.

‘Mikoa mingi hapa nchini ina upungufu wa vituo vya afya, zahanati na hospitali kubwa, ndio maana tumeona ipo haja ya kujenga kituo hicho cha matibabu mkoani hapa kama ambavyo tumedhamiria kufanya katika mikoa mingine pia’, alisema.

Aidha aliuomba uongozi wa serikali ya mkoa huo kushikamana na kuongeza hamasa kwa wananchi ili waweze kujiunga na kufaidi huduma mbalimbali za kiafya zitolewazo na mfuko huo.

Mkuu wa Mkoa huo Fatma Mwassa na Mkurugenzi mtendaji wa Manispaa hiyo Alfred Luanda walimhakikishia kuwa Manispaa hiyo iko tayari kushirikiana na mfuko huo sambamba na kutoa eneo kwa ajili ya ujenzi wa jengo la kitega uchumi na kituo cha matibabu kama mfuko huo ulivyokusudia.

Luanda aliwataka viongozi wote katika Manispaa hiyo kubadilika kiutendaji kwa kuongeza ufanisi katika kazi zao badala ya kuendekeza malumbano yasiyokuwa na tija ili kukabiliana na changamoto mbalimbali zilizopo katika Manispaa hiyo.

‘Manispaa yetu haishindwi kusajili idadi kubwa ya wanachama katika mfuko wa afya ya jamii-CHF, kinachotakiwa ni kubadilika tu kiutendaji na kuanza upya uhamasishaji wa wananchi’, aliongeza.

Katika mkutano huo wajumbe walipendekeza kiwango cha mchango wa kujiunga katika huduma hizo za mfuko wa afya ya jamii kwa mwaka kiwe shilingi 10,000 kwa kichwa, gharama ambayo itamwezesha mhusika kupata huduma za afya katika kituo chochote kile mkoani humo kwa kutumia kadi maalumu ya tiba.

Mwisho



No comments:

Post a Comment