Saturday, August 10, 2013

EID-EL-FITRI YAFANYIKA KITAIFA TABORA,MAKAMU WA RAIS AHIMIZA UMOJA NA MSHIKAMANO

NA LUCAS RAPHAEL,TABORA 

 
WAUMINI wa dini ya kiislam hapa nchini wametakiwa kuuenzi mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani kwa kudumisha amani, upendo na mshikamano kwa makundi ya watu wote ili thawabu walizopata katika mfungo huo zizidi kuongezeka.

Rai hiyo imetolewa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Dr. Mohamed Gharib Bilal aliyekuwa mgeni rasmi katika
sherehe za Idd el-Fitri zilizofanyika kitaifa jana katika uwanja wa
Ali Hassan Mwinyi mkoani Tabora.

Dr. Bilal alisema kuwa katika mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani waumini wa dini hiyo wamepata mafunzo mengi  yaliyoambatana na matendo mema kwa jamii, hivyo akawasihi wachukue mafunzo hayo ya Mwenyezi Mungu kama dira ya maisha yao ili kudumisha amani, upendo na mshikamano miongoni mwa jamii kwani hayo ndiyo chachu kubwa ya ustawi na maendeleo ya Watanzania wote.

‘Ndugu zangu naomba tuchukue na kuyaenzi mafunzo yote tuliyopata
katika mwezi huu mtukufu kwa kuendeleza matendo mema, kutoa sadaka kwa watu wenye uhitaji, kuonyesha ukarimu kwa makundi mbalimbali ya watu wakiwemo  wagonjwa na watoto wadogo’ alisema.

Aidha, Dr. Bilal aliongeza kuwa ili kudumisha amani katika nchi yetu
na katika jamii nzima inayotuzunguka hatuna budi kupendana,
kuheshimiana na kushikamana kwa kuwa sisi sote ni wamoja, na kwa
kufanya hivi jamii ya kimataifa itaendelea kutuheshimu na kututhamini
zaidi.

Awali, Mufti wa Tanzania, shekhe Issa Shaaban Simba, akimkaribisha
Makamu wa Rais kuzumgumza na wananchi katika ibada hiyo, alisifu
waumini wa dini hiyo kwa kujitokeza kwa wingi katika sherehe hiyo ya
kuhitimisha mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani kwa amani.

Shekhe Mkuu wa Mkoa wa Tabora, shekhe Shaban Salumu, akitoa salaamu za mkoa, alisema kuwa mwezi mtukufu wa Ramadhani ni fursa pekee yenye kheri na thawabu kubwa kwa waumini wa dini ya kiislam, hivyo akawataka waumini hao wasipoteza thawabu hizo bali waendelee kumcha mwenyezi Mungu ili wapate kufanikiwa zaidi.

Naye Diwani wa kata ya Chemchem iliyopo katika manispaa ya Tabora,Ikunji Furaha Hassan, alipongeza maandalizi mazuri yaliyofanywa na serikali ya mkoa huo ambayo yamefanikisha sherehe hizo kwa kiwango kikubwa sana, na aliwataka wananchi wote kusherehekea sikukuu hiyo kwa amani.

Baadhi ya waumini wa dini ya kiislamu walioshiriki Ibada ya Sala ya Eid El Fitri iliyofanyika kitaifa mkoani Tabora.
Makamu wa Rais Dr.Gharib Bilali akizungumza na waislamu katika Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi ambapo aliwataka kudumisha amani na mshikamano pasipo kujali dini,Rangi wala kabila.
Sheikh wa mkoa wa Tabora Shabani Salumu wakati akisoma hotuba ya Sala ya Eid -El Fitri iliyofanyika kitaifa mkoani Tabora.
Baadhi ya Waumini wa dini ya kiislamu mjini Tabora wakisikiliza kwa makini Hotuba ya Sala ya Eid El Fitri.
Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Tabora mjini Bw.Moshi Nkokota ambaye alinaswa na Kamera Yetu katika Sala hiyo ya Eid El Fitri.
Makamu wa Rais Dr.Gharib Bilal akimsalimia  Sheikh mkuu wa Tanzania Mufti Issa  Shaaban Simba mara baada ya Sala ya Eid El Fitri iliyofanyika uwanja wa Ali Hassan  Mwinyi.
Mufti Issa Shaaban Simba akiomba dua ya pamoja baada ya Sala ya Eid El Fitri.
Waumini wa dini ya Kiislam wakimuaga Sheikh mkuu wa Tanzania wakati akiondoka uwanjani hapo baada ya Sala.





No comments:

Post a Comment