Monday, June 17, 2013

JITIHADA ZA MKUU WA MKOA TABORA ZAANZA KUWANUFAISHA VIJANA


 
NA LUCAS RAPHAEL-SIKONGE  
JITIHADA za mkuu wa mkoa wa Tabora Bi. Fatma Mwassa kuhakikisha mkoa huo unakuwa na kituo cha kisasa cha mafunzo ya ujasiriamali kwa vijana ili kuboresha maisha yao zimeanza kuzaa matunda baada ya kituo hicho kuanza kutoa mafunzo mbalimbali kwa vijana kutoka maeneo mbalimbali katika wilaya ya Sikonge mkoani humo.
Hayo yalibainishwa jana katika ziara maalumu iliyofanywa na mkuu huyo wa mkoa akiambatana na watendaji wakuu wa serikali ya mkoa na halmashauri ya wilaya ya Sikonge walipotembelea kituo hicho na kushiriki kazi mbali mbali pamoja na vijana walioko katika kambi hiyo.
Katika ziara hiyo Bi. Mwassa na wasaidizi wake walishuhudia shughuli mbalimbali zilizofanywa na vijana hao kwa ustadi mkubwa katika kituo hicho ikiwemo ubunifu wa kutengeneza vitu mbalimbali, utengenezaji na utundikaji wa mizinga ya nyuki, ujenzi wa mabanda ya kufugia nyuki, ufyatuaji matofali aina ya ‘interlock’, bustani za mboga mboga katika mtindo wa ‘green-house’, useremala na mengineyo.
Akiwa katika kituo hicho ambacho kutokana na umaarufu wake vijana hao wamekipa jina la ‘TULU GREEN CITY’, Mwassa alisema kuwa mpaka sasa vijana hao wamefanya mambo makubwa kwa mda mfupi  jambo linaloashiria mwanzo mzuri huku akiwapongeza wataalamu wote wanaowasaidia vijana hao.
Aidha, Mwassa aliongeza kuwa vitu vyote vitakavyotengenezwa na vijana hao vitakuwa vikiuzwa kwa watu mbalimbali ikiwemo halmashauri zote za mkoa huo ili kuwanufaisha zaidi vijana hao na kwa kuanzia tayari tumeshapokea oda toka sehemu mbalimbali za kununua matofali hayo na vifaa vingine vitakuwa vikiuzwa katika maonesho ya kibiashara.
Aidha , Mwassa alibainisha kuwa Tanzania tumeamua kuingia kwenye mfumo wa matokeo makubwa sasa  unaojulikana kwa jina la ‘BIG RESULTS NOW’  lengo likiwa kuwapa vijana ujuzi katika nyanja mbalimbali ili wawe chachu ya maendeleo kupitia uzalishaji na utengenezaji wa bidhaa kadhaa wa kadha sambamba na kuwafundisha vijana wenzao.
Mwassa alibainisha kuwa nguvu kazi ya vijana hao imeanza kuiva, kazi zinafanyika kwa uhakika na matumaini juu ya vijana hao ni makubwa, na kuongeza kuwa kuanzia mwezi Desemba mwaka huu wanatarajia kuanza ufugaji, kilimo cha mtama, alizeti, viazi vitamu, mbogamboga na mazao mengine yanayostahimili ukame sambamba na ujenzi wa jengo la utawala na karakana.
 ‘Hii ni fursa muhimu sana kwa vijana wetu wasiipoteze, naomba wana Tabora waniunge mkono ili ndoto zangu za maendeleo kwa vijana na mkoa kwa ujumla zitimie na hatimaye tubadilishe uzalishaji katika mkoa huu’, alisema.
Akizungumza na waandishi wa habari katika kituo hicho, Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Sikonge Robert Kamoga, alipongeza wazo la kuanzishwa kituo hicho katika wilaya hiyo na kubainisha kuwa kero za ajira kwa vijana sasa zitapungua kwa sababu vijana hao watajiajiri wenyewe na kuajiri vijana wenzao, hivyo akatoa wito kwa jamii kutembelea kituo hicho ili kujifunza.
Naye Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Sikonge Shedrack Mhagama, alisema kuwa wamedhamiria kuwawezesha vijana kupata ujuzi utakaowawezesha kutengeneza ajira zao wenyewe ili kujiongezea kipato kupitia uzalishaji mali, ufugaji wa ng’ombe, mbuzi na kuku, kilimo na ujenzi, hivyo akawashauri wazazi wawaruhusu vijana wao wajiunge na kituo hicho.
Vijana walioko katika kituo hicho Remi Alisemi (22) na Raymond Peter (23) wakizungumza mbele ya mkuu wa mkoa, walitoa shukrani zao kwa kuanzishwa kijiji hicho cha mfano na kusema kuwa kimekuwa mkombozi wa maisha yao kwani awali walikuwa wazururaji tu huku wengine wakiwa wavuta bangi, vibaka, wabwia unga na hawakuwa na ujuzi wowote ule tofauti na walivyo sasa.

No comments:

Post a Comment