Saturday, July 13, 2013

WATOTO SABA RAIA WA BURUNDI NA RWANDA WASALIMIKA KUUZWA TABORA


Watoto saba  ambao ni raia  wa  Burundi na Rwanda ambao walikamatwa wakati walipokuwa wakisafirishwa kutoka Burundi kuja Tabora kwa ajili ya kuuzwa watumikishwe katika mashamba  ya tumbaku,Watoto hawa walikamatwa  eneo  la  Ulyankulu wilayani  Kaliua wakiwa na  tajiri  yao ambaye amefahamika kwa jina la Emmanuel John(22) ambaye pia ni raia wa Burundi. 
Watoto  wakiwa mahakama ya hakimu mkazi Tabora  wakisubiri kuingia mahakamani kutoa ushahidi baada ya mtu aliyekuwa amewasafirisha kwa lengo la kutaka kuwauza kukamatwa na kufikishwa Mahakamani kujibu shitaka la kuwasafirisha kwa nia ya kuwafanyia biashara na kuingia nchini kinyume cha sheria.
Afisa na Mwanasheria wa Idara ya Uhamiaji mkoa wa Tabora  akiwaongoza watoto hao kuingia chumba cha mahakama ya hakimu mkazi Tabora kwa ajili ya kutoa ushahidi dhidi ya Emmanuel John.

  NA LUCAS RAPHAE,TABORA
 
RAIA wa Burundi, Emmanuel John (22),aliyekamatwa akituhumiwa kusafirisha watoto,amefikishwa katika Mahakama ya Mkoa waTabora akikabiliwa na Mashitaka mawili moja likiwa ni la kuingia nchini kinyume cha sheria na kusafirisha binadamu kwa lengo la kutaka kuwauza.
 
Mbele ya Hakimu Mkazi Bw. Jackton Rushwela,Wakili wa Serikali Bw.Iddi Mgeni, alimsomea mshitakiwa mashitaka hayo ambapo alikiri kosa la kuingia nchini kinyume cha sheria huku kosa la pili la kuwasafirisha watoto hao saba  akijaribu kutaka kuficha ukweli.
Kutokana na kukiri kosa la kwanza, Hakimu Rushwela
alimhukumu kifungo cha mwaka mmoja jela au kulipa faini ya sh 100,000. 
Hata hivyo,mshitakiwa huyo Emmanuel John pamoja na kuiomba mahakama impatie fursa ya kumtaarifu mkewe aliyeko huko nyumbani kwao nchini Burundi kwa njia ya simu au apewe nafasi ya kuuza simu yake ya mkononi aweze kulipa faini hiyo kwa nia ya kutaka kujinasua na adhabu ya kifungo hicho cha mwaka mmoja lakini mahakama haikuwa tayari kutekeleza hilo. 
Kuhusu shitaka la kusafirisha binadamu,upande wa mashitaka ulidai mshtakiwa alikamatwa na maofisa wa Idara ya Uhamiaji akiwasafirisha watoto Ndayisenga Batiliza(13),
Ndakusenga Emmanuel(15), Nimbonajile Nagenda(13),
Yazid John(15), James Justus(14) na Samson Banteke(17). 
Baadhi ya watoto hao walitoa ushahidi walidai walisafirishwa na mshitakiwa Emmanuel John kutoka nchini Burundi na Rwanda hadi walipokamatwa eneo  la  Ulyankulu  wilayani Kaliua.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Julai 25, mwaka huu itakapoendelea tena kusikilizwa kwa mashahidi wengine kutoa ushahidi wao. 

No comments:

Post a Comment