Sunday, December 23, 2012

JUHUDI ZA SERIKALI KUTANGAZAO UKEZAJI ZAFANIKIWA


Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) Bw. Raymond Mbilinyi, (kushoto) akifurahia jambo na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uwekezaji Huru Tanzania (EPZA) Dkt. Adelhelm Meru muda mfupi mara baada ya kukutana na ujumbe wa wawekezaji kutoka nchini china mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam.
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) Bw. Raymond Mbilinyi, (kushoto) akifurahia jambo na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uwekezaji Huru Tanzania (EPZA) Dkt. Adelhelm Meru muda mfupi mara baada ya kukutana na ujumbe wa wawekezaji kutoka nchini china mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam.
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Juhudi za serikali kutangaza vivutio vyake vya uwekezaji zinazidi kuzaa matunda baada ya ujio wa ujumbe wa watu sita wa kampuni ya Anhui Foreign Economic Construction ya nchini China kuja nchini kujionea na kujua fursa mbalimbali wanazoweza kuwekeza hapa nchini.

Akiongea na waandishi wa habari kuhusiana na ujio huo, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), Bw. Raymond Mbilinyi alisema ujumbe huo ni wa wawekezaji wakubwa kutoka China wanaotaka kuwekeza hapa nchini kwa ushirikiano na serikali ya Tanzania.

“Hii ni fursa nyingine ambayo nchi inapata kupitia uwekezaji, hawa ni wawekezaji wakubwa ambao wamekuja kwa lengo la kuangalia fursa mbalimbali hapa nchini,” alisema Bw. Mbilinyi mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam.

Aliongeza kuwa ujumbe huounaoongozwa na mwenyekiti wake wa bodi, Bw. Jiang Qingde umeshaonana na Rais Jakaya Kikwete na kuzungumza naye mambo mbalimbali juu ya ujio wao hapa nchini.

“Ni kampuni yenye uzoefu wa hali ya juu katika sula la uwekezaji,” alisema.

Akielezea zaidi alisema mpaka sasa wamewekeza katika nchi zipatazo 20 katika bara la Afrika hivyo kuja kwao hapa nchini ni ishara kuwa Tanzania pia ina mazingira mazuri ya uwekezaji na kwamba jitihada za TIC kutangaza fursa za uwekezaji hapa nchini zinazaa matunda.

Alisema kuwa wawekezaji hao wana uzoefu mkubwa katika sekta za madini, viwanja vya ndege, na nishati ya umeme.

Alisema kwa upande wa viwanja vya ndege tayari kampuni hiyo imeweza kuwekeza katika katika nchi 15 katika bara la Afrika, na kuongeza kuwa wana uzoefu wa kutosha katika suala la uwekezaji katika maeneo mengi ya Afrika.

Alisema kuwa uzoefu walionao wawekezaji hao utasaidia sana katika sula la kukuza uchumi wa nchi na kuongeza ajira hapa nchini kwa kuwa uwekezaji wao ni wa maeneo mengi kwa wakati mmoja hivyo ni fursa ya kipekee kwa nchi katika kutengeneza ajira kupitia sekta ya uwekezaji toka nje.

“Kuna tatizo la ajira kwa vijana wetu, hivyo kuwepo kwa fursa za uwekezaji hapa nchini ni jambo jema kwa serikali yetu kuondokana na tatizo hili kwa kiasi kikubwa,” alisema Bw. Mbilinyi na kuongeza kuwa TIC itaendelea na juhudi zake za kutangaza vivutio vya uwekezaji Tanzania kwa wawekezaji wa ndani na nje.

Tanzania ina mahusiano mazuri ya kijamii na kiuchumi na watu na serikali ya China.

Kampuni mbalimbali toka nchi hiyo ambayo inapiga hatua kubwa kiuchumi kwa kasi zimekua zikifanya kazi hapa Tanzania kwa miaka kadhaa hasa katika sekta ya ujenzi wa vitu mbalimbali.

No comments:

Post a Comment