Sunday, December 23, 2012

KITUMBO MWENYEKITI MPYA TAREFA


 
Na Lucas Raphael,Tabora

CHAMA soka mkoa wa Tabora,(TAREFA),kimefanya mkutano wake mkuu na kuchagua viongozi  ambao watakaa madarakani kwa kipindi cha miaka minne.

 
Uchaguzi huo ulifanyika katika ukumbi wa mikutano wa mamlaka ya maji safi na maji taka,mjini Tabora,TUWASA.
 
Akitangaza matokeo ya uchaguzi huo mwenyekiti wa kamati ya uchaguzi Bwire Mkama,alisema nafasi ya mwenyekiti ilikuwa na wagombea watatu ambapo Yusuph Kitumbo alishinda kwa kura (16), akifuatiwa na Mussa Ntimizi kura (8), huku meneja wa TRA Tabora akipata kura (0) ambapo kura halali zilizopigwa ni 24 na hakukuwa na kura hata moja iliyoharibika.
 
Mkama aliongeza kuwa nafasi ya katibu wa TAREFA ilikuwa na wagombea wawili ambapo Fath Remtullah Dewij alishinda kwa kura (17), na kumshinda katibu wa TAREFA zamani Albert Sitta aliyepata kuwa (7) kura zilizopigwa 24.
 
Mwenyekiti huyo wa kamati ya uchaguzi alitangaza nafasi mwakilishi wa vilabu ilikwenda kwa Lazack Ilumba akishinda kwa kura (13),huku nafasi mjumbe wa mkutano mkuu TFF ikienda kwa Dick Mlimuka aliyepata kuwa (14).
 
Mkama alimtangaza mshindi wa nafasi ya mwakilishi wa soka la wanawake ambaye alikuwa mgombea pekee Janeth Michael aliyepata kura (22),huku nafasi ya mjumbe kamati ya utendaji ikienda kwa Stanlaus Shija aliyeshinda kwa kura (22).
 
Aidha mwenyekiti wa kamati ya uchaguzi alitamka kuwa nafasi kadhaa bado ziko wazi kwa kukosa wagombea huku nafasi moja mgombea akijitoa kwa kutingwa na majukumu mengi.
 
Mkama alitaja nafasi zilizowazi kuwa ni nafasi ya makamu mwenyekiti,katibu msaidizi,mjumbe wa kamati ya utendaji na mweka hazina msaidizi huku nafasi ya mweka hazina Musa Msananga akijitoa kwa kuandika barua akidai kutingwa na majukumu ya kikazi.
 
Mwenyekiti mpya wa TAREFA aliyeshinda uchaguzi huo Yusuph Kitumbo katika nasaha zake alisema anavunja makundi yote ili kujenga uongozi imara wenye kutaka kuleta maendeleo ya soka mkoa wa Tabora.
 
Kitumbo aliongeza moja kazi zake atakazoanza nazo ni pamoja na kuhakikisha chama kinakuwa na ofisi ya kisasa inayotambulika.
 
Aidha aliongeza kuwa kazi nyingine ni kuhakikisha uongozi wa wilaya nao unatimiza majukumu yao ipasavyo na sanjari na kuwa na ofisi zinazoeleweka.
 
Alisema atahakikisha vikao vyote vya kikatiba vinafuata taratibu na kalenda kamwe hatakuwa mtu wa makundi daima atahakikisha upendo mshikamano na utulivu vinakuwepo miongoni mwa viongozi walioshinda na wagombea wote walioanguka kwenye uchaguzi huo atashirikiana nao pia.
Hata hivyo baadhi ya wadau wa soka mkoani Tabora macho na masikio yao kwasasa wamemuangazia Yusuph Kitumbo ili kuona kama atakuwa na uwezo wa kuleta mabadiliko ya kweli kwa Chama hicho.  

No comments:

Post a Comment