Thursday, December 27, 2012

Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar na Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi CUF Maalim Seif Sharif Hamad:'Mwaka wa 2012 ni mwaka wa historia'

   Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar na Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad akiwahutubia wafuasi wa chama hicho katika mkutano wa kufunga mwaka uliofanyika viwanja vya Kibandamaiti.
Mwakilishi wa Jimbo la MjiMkongwe Zanzibar Ismail Jussa Ladhu (CUF), akiwahutubia wafuasi wa chama hicho katika mkutano wa kufunga mwaka uliofanyika viwanja vya Kibandamaiti.
   Kaimu Naibu Katibu Mkuu wa CUF Zanzibar Hamad Massoud Hamad, akiwahutubia wafuasi wa chama hicho katika mkutano wa kufunga mwaka uliofanyika viwanja vya Kibandamaiti.
  Wafuasi na wapenzi wa CUF wakiwa katika mkutano wa kufunga mwaka ulioandaliwa na chama hicho katika viwanja vya Kibandamaiti.
  Wafuasi na wapenzi wa CUF wakiwa katika mkutano wa kufunga mwaka ulioandaliwa na chama hicho katika viwanja vya Kibandamaiti.Picha na Salmin Said-Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar
--
Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar na Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi CUF Maalim Seif Sharif Hamad amesema mwaka 2012 umekuwa na umuhimu wa kipekee katika historia ya kisiasa Tanzania.
Amesema ndani ya mwaka huu unaomalizika Watanzania katika mikoa yote wamepata fursa ya kutoa maoni yao juu ya uundwaji wa katiba mpya ya Tanzania ambayo yatatoa mwelekeo imara wa mustakbali wa nchi.
Maalim Seif ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar ametoa kauli hiyo mwishoni mwa wiki wakati akihutubia mkutano maalum wa hadhara wa Chama hicho kwa ajili ya kuuaga mwaka 2012, uliofanyika viwanja vya Kibandamaiti Zanzibar.

Amesema suala la kuwashirikisha wananchi katika jambo kubwa kama hilo la kuamua juu ya mustakbali wa nchini yao ni la kihistoria, na kutaka maoni ya wananchi wa pande mbili za Muungano yathaminiwe na yaheshimiwe.
 
Amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete kwa kubariki uundwaji wa katiba mpya ya Tanzania na kuwashirikisha wananchi, suala ambalo lilikosekana katika awamu zilizopita za uongozi.
 
“Nachukua fursa hii kumpongeza sana Rais Kikwete kwa kubariki jambo hili, wakati wa marehemu Mwalimu Nyerere ilionekana kama uhaini kuzungumzia masuala ya Muungano hadharani lakini leo hii kila mwananchi anayo haki ya kuujadili kabisa”,alieleza Maalim Seif na kuongeza kuwa hiyo ni hatua kubwa zaidi ya kisiasa kuwahi kufikiwa Tanzania.
 
Ameuombea mwaka mpya wa 2013 uwe wa neema ambao utaisababishia Zanzibar kusonga mbele katika kufikia malengo yake iliyojipangia.
 
Maalim Seif amewashuku wananchi wa Zanzibar kwa kuonyesha mshikamano wakati wa utoaji wa maoni, na kwamba umoja wa Wazanzibari ndio utakaopelekea kupatikana kwa Zanzibar yenye mamlaka kamili ndani na nje ya Zanzibar.
 
Kwa upande wake Kaimu Naibu Katibu Mkuu wa CUF Zanzibar Hamad Massoud Hamad amesema chama chake kinajipanga kwa ajili ya kupata ushindi mkubwa katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.
Amewaomba wananchi kuendelea kukiunga mkono chama hicho ili kiweze kutatua kero ya ukosefu wa ajira unaowakabili vijana wengi wa Zanzibar.
 
“Vijana wengi wa Zanzibar bado hawana ajira, vijana hawa wamesoma wengine hadi vyuo vikuu na wazee wao wametumia fedha nyingi kuwasomesha lakini wapi, ajira imeota mbawa”,alisema Hamad Massoud.
 
Nae Mwakilishi wa Jimbo la Mjimkongwe Ismail Jussa Ladhu, amesewa Wazanzibar wameitumia vyema fursa yao ya kutoa maoni, tofauti na ilivyoelezwa na baadhi ya wajumbe wa Tume wa kukusanya maoni.
 
Amefahamisha kuwa maoni waliyoyatoa Wazanzibari ni sahihi na wala hawakupoteza fursa hiyo kama ilivyodaiwa, ikizingatiwa kuwa suala la msingi kwa Zanzibar ndani ya Muungano ni “Muungano wenyewe” kwa vile Zanzibar ina katiba yake ambayo imeweka wazi juu ya masuala yote yanayohusu nchi ya Zanzibar.

 Na 
Hassan Hamad 
Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar

No comments:

Post a Comment